Pages

Subscribe:

Thursday, 8 October 2015

AGANO LA SABATO

WAKRISTO WENYE IMANI YA SABATO Neno SABATO linatokana na neno la lugha ya Kiebrania liitwalo SHABBATH, au SABBATON kwa lugha ya Kiyunani, likiwa na maana ya "KUKOMA, au KUTULIA, au KUSTAREHE au PUMZIKO." Kwa asili SABATO ilianzia pale Mungu alipomaliza kazi ya uumbaji. Biblia Takatifu inasema kwamba: "Na siku ya saba Mungu alimaliza kazi yake yote aliyoifanya; akastarehe siku ya saba, akaacha kufanya kazi yake yote aliyoifanya. Mungu akaibarikia siku ya saba, akaitakasa kwa sababu katika siku hiyo Mungu alistarehe, akaacha kufanya kazi yake yote aliyoiumba na kuifanya." - (Mwanzo 2:2-3) Kama tulivyotangulia kujifunza maana ya SABATO ni "KUKOMA, au KUTULIA, au KUSTAREHE, au PUMZIKO" ndiyo maana tumeona "...Mungu alistarehe, akaacha kufanya kazi yake yote aliyoiumba..." - (Mwanzo 2:2-3). Mungu mwenyewe alipumzika "...alistarehe..." baada ya kumaliza kazi Yake ya uumbaji. Kutokana na umuhimu wa kupumzika Kwake; Mungu akaitakasa siku hiyo ya saba. Neno "TAKASA" maana yake ni "KUWEKA WAKFU au KUTENGA KWA AJILI YA MATUMIZI MATAKATIFU. Baada ya uumbaji, kuanzia wakati wa Adamu hadi Yusufu mwana wa Yakobo (Israeli), kwa wakati huo wanadamu hawakuwa na amri ya kuiadhimisha siku ya SABATO. Kwao siku zote zilikuwa sawa. Lakini, SABATO kwa wana wa Israeli ilianzia wakati wa Musa. Biblia Takatifu inasema kwamba: "Ikumbuke siku ya Sabato uitakase. Siku sita fanya kazi, ...lakini siku ya saba ni Sabato ya BWANA, Mungu wako, siku hiyo usifanye kazi yo yote, wewe, wala mwana wako, wala binti yako, wala mtumwa wako, ...wala wanyama wako.., ..wala mgeni aliye ndani ya malango yako." (Kutoka 20:8-10) Hapo Mungu anampa Musa amri ya kuikumbuka siku ya Sabato kwa kutokufanya kazi yo yote yeye wala wana wa Israeli wala wageni wo wote walio katika miji yao. Mungu alisema hivyo kwa sababu kuu mbili, nazo ni zifuatazo: (a) Kuiweka siku hiyo kwa ajili ya kumwabudu Mungu badala ya wana wa Israeli kuitumia siku hiyo kwa kazi zao binafsi. (b) Wapumzike kutokana na kazi walizozifanya kwa mfululizo wa siku sita ili wapate nguvu mpya itakayowaongezea ufanisi wa kufanya kazi katika siku sita nyingine zinazofuatia. Hilo ndilo lilikuwa lengo la Mungu kuwaambia wana wa Israeli wawe na siku ya SABATO (PUMZIKO). Tunapozungumzia Sabato ya wana wa Israeli, ni pana sana na inaadhimishwa tofauti kabisa na jinsi ambavyo wanafanya Wasabato wa leo. Kwa wana wa Israeli, siku ya Sabato iliwekwa wakfu kwa ajili ya Mungu, ilikuwa ishara kwamba watu wale waliunganishwa na Mungu kwa njia ya Agano (mapatano). Vile vile Sabato ya wana wa Israeli haikuwa Sabato ya siku tu (yaani kupumzika tu katika kila siku ya saba ya juma), bali wana wa Israeli walikuwa na SABATO YA SIKU (kupumzika siku ya saba ya kila juma,) walikuwa na MWAKA WA SABATO, na pia walikuwa na SABATO YA MASHAMBA. Sabato hizo zote zina sheria zake ambazo walilazimika kuzitekeleza.  Sabato kwa wana wa Israeli ilikuwa ni ifuatavyo: i/: Mtu aliyefanya kazi siku hiyo alihukumiwa kifo. Ni marufuku kabisa kufanya kazi siku ya Sabato. Kulingana na torati, ni marufuku mtu kufanya kazi yo yote katika siku ya Sabato. Endapo mtu ye yote akikiuka agizo hilo, alihukumiwa adhabu ya kifo (aliuawa). Mungu anasema kwamba: "Basi mtaishika hiyo Sabato; kwa kuwa ni takatifu kwenu; kila mtu atakayeitia unajisi hakika yake atauawa; ...Kila mtu atakayefanya kazi yo yote katika siku ya Sabato, hakika yake atauawa." - (Kutoka 31:14-15) Hayo ndiyo maneno ya Mungu Mwenyewe wala si maneno yangu mimi au ya Musa, bali ni Mungu Mwenyewe. Kwa kila mtu aliyeinajisi Sabato; hapakuwa na majadiliano wala kuomba msamaha, bali hukumu hiyo utolewa hapo hapo. Na pia kwa msisitizo neno la Mungu linasema: "...wana wa Israeli wataishika Sabato, kuiangalia sana hiyo Sabato katika vizazi vyao vyote, ni agano la milele." - (Kutoka 31:16) Hadi hapo napenda niulize swali. Je! Wasabato wa leo wanawaua watu wote wafanyao kazi yo yote katika siku ya Sabato? Je! Wasabato wa leo wanaua kila mtu anayenajisi siku ya Sabato? Je! Wasabato wa leo wanatii amri ya Mungu au wameshika mafundisho ya nani? Majibu yote tutayafahamu huko mbeleni katika somo hili. Sheria nyingine ya Sabato ni hii ifuatayo: ii/: Wanyama wote wa kufugwa watumikao katika kufanya kazi; mfano farasi, ng'ombe, punda, n.k pia nao walipaswa kupumzika siku ya Sabato. Neno la Mungu linasema kwamba: "...siku ya saba ni Sabato ya BWANA, Mungu wako, siku hiyo usifanye kazi yo yote, wewe, wala mwana wako, wala binti yako, wala mtumwa wako, wala mjakazi wako, wala mnyama wako wa kufuga, wala mgeni aliye ndani ya malango yako." - (Kutoka 20:10) Kwahiyo si wanyama tu waliopaswa kupumzika kwenye siku ya Sabato, bali pia wote hawa walitakiwa wasifanye kazi: "...wewe, wala mwana wako, wala binti yako, wala mtumwa wako, wala mjakazi wako, wala mnyama wako wa kufuga, wala mgeni aliye ndani ya malango yako." Hivyo ndivyo jinsi sheria ya Sabato ilivyo. Labda niulize swali: Je! Wasabato wa leo wanafanya hivyo?  iii/: Nchi ya mashamba, ilipumzishwa baada ya kulimwa kwa mfululizo wa miaka sita. Ule mwaka wa saba unaitwa mwaka wa Sabato kwa ajili ya mashamba. Neno la Mungu linasema kwamba: "Panda shamba lako miaka sita, ...na kuyachuma matunda yake; lakini katika mwaka wa saba itakuwa ni Sabato ya kustarehe kabisa kwa ajili ya hiyo nchi, ...usipande shamba lako, wala usipelee shamba lako... Hicho kimeacho chenyewe.., usikivune, ...utakuwa mwaka wa kustarehe kabisa kwa ajili ya hiyo nchi." - (Walawi 25:3-5) Hapo tunaona Mungu anasema "...mwaka wa saba itakuwa ni Sabato ...usipande shamba lako, wala usipelee shamba lako...utakuwa mwaka wa kustarehe kabisa kwa ajili ya hiyo nchi." Niulize swali jingine tena hapa: Je! Wasabato wa leo wanafanya hivyo?  Kama jibu ni "HAWAFANYI HIVYO." Je! Nani amewapa amri ya kupunguza sheria za Mungu kwa kuchagua yale machache wayatakayo alafu wakayaboresha? Je! Huko ni kushika sheria ya Mungu au ni kushika mafundisho ya wanadamu? Sheria nyingine ya Sabato ni hii ifuatayo: iv/: Kuwasamehe wenye madeni wote unao wadai. Hiyo ni amri wala si hiari. Mungu anasema kwamba: "Kila miaka saba, mwisho wake, fanya maachilio. Na jinsi ya maachilio ni hii, kila mkopeshaji na akiache alichomkopesha mwenzake, wala asimlipize mwenziwe wala nduguye; kwa kuwa imepigwa mbiu ya maachilio ya BWANA." - (Kum 15:1-2) Hapo neno "...maachilio..." limetumika kumaanisha "...samehe..." kila deni unalodai kwa ndugu yako au kwa mwenzako ye yote yule. Ndiyo maana hapo Mungu anasema: "...kila mkopeshaji na akiache alichomkopesha mwenzake, wala asimlipize mwenziwe wala nduguye..." Mbiu hiyo ya maachilio hupigwa kila mwishoni mwa miaka saba. Hapa napo tena niulize swali: Je! Wasabato wa leo wanafanya hivyo? Na pia, Sheria nyingine ya Sabato ni hii ifuatayo: v/: Makuhani katika mwaka wa Sabato, walipaswa kuwakusanya watu wote kwa ajili ya kuwasomea sheria (Torati) hadharani, ili kuwakumbusha watu wajibu wao kwa Mungu. Masomo yale yalitekelezwa mahali rasmi pa ibada ambapo watu walikusanyika ili washerehekee sikukuu ya Vibanda. Biblia inasema: "Musa akaiandika torati hii, akawapa makuhani, ...na wazee wote wa Israeli. ...akawaamuru, ...Mwisho wa kila mwaka wa saba, wakati wa maachilio, wakati ulioamriwa wa sikukuu ya vibanda, ...Wakusanye watu, wanaume na wanawake na watoto, na mgeni ...wapate kusikia na kujifunza, na kumcha BWANA, Mungu wenu, na kuangalia kutenda maneno yote ya torati hii..." - (Kum 31:9-13) Biblia Takatifu inaposema "...WAPATE KUSIKIA NA KUJIFUNZA, ...NA KUANGALIA KUTENDA MANENO YOTE YA TORATI HII..." Maana yake ni kwamba kila kilichomo ndani ya torati ni lazima kukitekeleza pasipo kupunguza neno wala kuongeza neno. Je! Wasabato wa leo wanafanya hivyo? SABATO ni amri inayopatikana ndani ya TORATI. Na pia tunapozungumzia “TORATI” maana yake ni “SHERIA” yote ambayo ndani yake tunakuta kipenyere cha Sabato. Kwa maneno ya sasa tunaweza kuifananisha TORATI na KATIBA alafu SABATO ni IBARA iliyomo ndani ya KATIBA. Biblia inalitumia neno TORATI au SHERIA kwa mtazamo mbali mbali; Upo wakati limetumiwa kwa maana ya amri au maagizo na maelezo ya jumla ambayo yametolewa na Mungu, au na wazazi, serikal, au walimu (Mwa 26:5; Kut 18:20; Zab 119:18-20, 51-61; Mhu 3:1; 6:20), mara nyingine linahusika kutaja Agano la Kale kwa ujumla, na pia mara nyingine linakuwa linataja kwa sehemu ya Agano la Kale tu hususani vile vitabu vitano vya Musa (Mt 5:17; Lk 24:44; Yn1:45; 15:25) ambavyo vilijulikana kwa jina la PENTATUKI. Jina hili "PENTATUKI" linatokana na maneno mawili ya lugha ya Kiyunani (Kigiriki) nayo ni "PENTA" maana yake ni "TANO", na neno "TEUCHOS" maana yake ni "KITABU". Waebrania waliiita PENTATUKI yote SHERIA au TORATI. Vitabu hivyo ni MWANZO (GENESIS), KUTOKA (EXODUS), WALAWI (LEVITICUS), HESABU (NUMBER) na KUMBUKUMBU LA TORATI (DEUTERONOMIUM). Hiyo ndiyo  maana halisi ya TORATI au SHERIA ilivyo ki mtazamo wa Biblia. Kwa hiyo tumeona Biblia inasema: "Musa akaiandika torati hii, akawapa makuhani, ...na wazee wote wa Israeli. ...akawaamuru, ...Mwisho wa kila mwaka wa saba, wakati wa maachilio, wakati ulioamriwa wa sikukuu ya vibanda, ...Wakusanye watu, wanaume na wanawake na watoto, na mgeni ...wapate kusikia na kujifunza, na kumcha BWANA, Mungu wenu, na kuangalia kutenda maneno yote ya torati hii..." - (Kum 31:9-13) Torati hiyo ni maagizo na amri zote zilizomo katika vitabu vyote vitano (PENTATUKI); hiyo ndiyo ambayo waliamuriwa kuishika pasipo kuongeza wala kupunguza neno lo lote lile. Pia tunaona Mungu anamwambia Musakwamba: "Wakusanye watu, wanaume na wanawake na watoto, na mgeni wako aliyemo malangoni mwako wapate kusikia na kujifunza, na kumcha BWANA, Mungu wenu, na kuangalia kutenda maneno yote ya torati hii." - (Kum 31:12) Maana yake ni kwamba, wote wanalazimika kusikia, kujifunza, kumcha Mungu, na kutenda maneno yote ya hiyo sheria ambayo Musa amepewa na Mungu. Endapo ukiishi kwa kushika torati / sheria ni makosa kabisa kubagua cha kushika kulingana na matakwa yako binafsi; kwa maana imeandikwa: "Na alaaniwe asiyeyaweka imara maneno ya torati hii kwa kuyafanya. Na watu wote waseme, Amina." - (Kum 27:26); na pia ni makosa kuongeza wala kupunguza neno lo lote lie ambalo Mungu ameamuru lifanywe. Kwa maana Mungu anasema: "Msiliongeze neno niwaamurulo wala msilipunguze, mpate kuzishika amri za BWANA, Mungu wenu, niwaamuruzo." - (Kum 4:2) Hivyo basi, Sabato ni moja kati ya amri za Mungu zilizomo ndani ya TORATI. Pia Sabato ni pana sana na inazo sheria zake kama jinsi tulivyojifunza hapo awali. Kwa maneno ya sasa tunaweza kuifananisha TORATI na KATIBA alafu SABATO ni IBARA iliyomo ndani ya KATIBA. Kwa mara nyingine tena niulize swali; Je, Wasabato wa leo wanatekeleza yote yaliomo ndani ya torati kama jinsi Mungu alivyo amuru? Endapo kama - Hawatekelezi! JE! ASILI YA WASABATO WA LEO NI IPI? Kumbuka Waswahili husema: "Ukweli usioujua hauwezi kukusaidia." Nami pia nasema kwamba: "Uongo usioujua ni vigumu kuuepuka." Lengo kuu la kujifunza ni kuifahamu kweli yote; Lakini zingatia kwamba: "Hauta elewa mpaka pale utakapo funguka akili; na hautafunguka akili mpaka pale utakapoikubali kweli." HISTORIA YA CHIMBUKO LA WASABATO WA LEO. Bila shaka kama umefatilia vizuri somo hili utakuwa unaelewa vizuri maana ya neno SABATO kwa mtazamo wa ki-Biblia. Sasa basi; Wasabato wa leo wanajulikana kwa jina la "Waadventista Wasabato" yaani "Seventh Day Adventists". Tofauti na Wakristo wengine: - Wasabato wa leo (SDA) wao siku yao ya ibada ni siku ya saba ya juma (Jumamosi ya kisasa ambayo kwa mujibu wa Biblia Takatifu ndiyo siku ya saba ya juma yaani SABATO).  - Woa wanazuiwa kula baadhi ya vyakula ambavyo vinaliwa na Wakristo wa madhehebu mengine. (huko mbeleni katika somo hili tutajifunza kuhusu vyakula). IMANI YA WASABATO WA LEO (SDA) ILIANZA KAMA IFUATAVYO: Waasisi (waanzilishi) wa imani hiyo ni: i/: William Miller Alizaliwa mwaka 1782 katika mji wa Pittsfield, Massachusetts, Marekani na alifariki mwaka 1849. Alizaliwa kwenye familia ya Kikristo lakini aliuacha (aliasi imani ya Ukristo) alipokuwa kijana. Hakuiamini Biblia Takatifu kuwa ni Neno la Mungu. Katika mwaka wa 1816 aliongoka na kuurudia Ukristo, akapenda kusoma unabii kwa kina uliohusu kurudi kwa Yesu Kristo. Kutokana na kujifunza kwake unabii, alishawishika kwamba mwisho wa dunia (Kiyama) ingakuwa mwaka wa 1843. Ulipofika mwaka 1831 alitangaza hadharani maono ya unabii aliokuwanao kuhusu mwisho wa dunia. Akapata umahalufu sana sehemu nyingi na hatimaye akawa mhubiri wa dhehebu la KIBAPTISTI. Kutokana na kwamba mwisho wa dunia unaambatana na kurudi kwa Yesu Kristo ambako kwa lugha ya Kiingereza huitwa "Christ's Advent", wafuasi wake walianza kujulikana kama "Adventists" au "Waadventista"; yaani "Watarajiao kurudi kwa Kristo." Ikumbukwe kwamba: William Miller alikuwa ni mhubiri wa dhehebu la KIBAPTIST, na hadi kufa kwake kamwe hakuwahi kuwa muumini wa dhehebu la Waadventista Wasabato (SDA) kwa sababu yeye alifariki hata kabla ya dhehebu hilo kuanzishwa; lakini mafundisho yake yamekuwa nguzo katika uasisi wa dhehebu la Waadventista Wasabato (SDA) kama jinsi tutakavyojifunza huko mbeleni katika somo hili. William Miller alikuwa ni Madventista wala si Msabato. William Miller alishawishika kufundisha kwamba mwisho wa dunia (Kiyama) ingekuwa mwaka 1843 kutokana na jinsi yeye alivyotafsiri andiko la kitabu cha DANIELI 9:24-27. Biblia Takatifu inasema: “Muda wa majuma sabini umeamriwa juu ya watu wako, na juu ya mji wako mtakatifu, ili kukomesha makosa, na kuishiliza dhambi, na kufanya upatanisho kwa ajili ya uovu, na kuleta haki ya milele, na kutia muhuri maono na unabii, na kumtia mafuta Yeye aliye mtakatifu. Basi ujue na kufahamu, ya kuwa tangu kuwekwa amri ya kutengeneza na kuujenga upya Yerusalemu  hata zamani zake Masihi aliye Mkuu; kutakuwa na majuma saba; na katika majuma sitini na mawili utajengwa tena pamoja na njia kuu zake na handaki, naam, katika nyakati za taabu. Na baada ya yale majuma sitini na mawili, Masihi atakatiliwa mbali, naye atakuwa hana kitu; na watu wa mkuu atakayekuja watauangamiza mji, na patakatifu; na mwisho wake utakuwa pamoja na gharika, na hata mwisho ule vita kuwepo; ukiwa umekwisha kusudiwa. Naye atafanya agano thabiti na watu wengi kwa muda wa juma moja; na kwa nusu juma hiyo ataikomesha sadaka na dhabihu; na mahali pake litasimama chukizo la uharibifu; na hivyo, hata ukomo, na ghadhabu iliyokusudiwa imemwagwa juu yake mwenye kuharibu.” - (Dan 9:24-27) Unabii huo wa Danieli unahusu majuma sabini yaliyowekwa kwa ajili ya watu wa Mungu, na mwanzo wa majuma hayo ni tangu kujengwa upya kwa mji wa Yerusalemu, hadi kukatiliwa mbali kwa Masihi.

KUANGUSHA NGOME YA MAWAZO

Mitume na manabii waliotangulia zamani tunaona kabisa kuwa walifanikiwa mbele za MUNGU baada tu
ya
kufanikiwa kuzijua mbinu za shetani
ambazo mara nyingi huzitumia kuachilia mawazo ndani ya mtu.

Aidha,
mgawanyiko wa mawazo haya una chimbuko lake maalum.

Mawazo chanya ambayo ni mema chimbuko lake ni Mungu ambaye amejitambulisha katika maandiko matakatifu ya Biblia; na mawazo hasi ambayo ni mabaya na maovu chimbuko lake ni Shetani na Ibilisi. Ninaposema chimbuko la “mawazo chanya” ambayo ni mema asili yake ni Mungu, hii ni kwa mujibu wa Biblia jinsi alivyomtafsiri Mungu kwamba anayo mawazo anayotuwazia binadamu wake kama livyoandikwa:

“Maana nayajua mawazo ninayowawazia ninyi, asema BWANA, ni mawazo ya amani wala si ya mabaya, kuwapa ninyi tumaini siku zenu za mwisho.” (Yer.29:11)

Aidha ninaposema “mawazo hasi” ambayo ni mabaya na maovu asili yake ni Ibilisi na Shetani, hiyo nayo ni kwa mujibu wa Biblia kama Yesu alivyomtambulisha Shetani kwetu akisema:

“Ninyi ni wa baba yenu, Ibilisi, na tamaa za baba yenu ndizo mpendazo kuzitenda. Yeye alikuwa mwuaji tangu mwanzo; wala hakusimama katika kweli, kwa kuwa hamna hiyo kweli ndani yake. Asemapo uongo, husema yaliyo yake mwenyewe; kwa sababu yee ni mwongo na baba wa huo.” (Yh.8:44) Unaona maneno kama haya ya “yeye ni mwuaji tangu mwanzo…” na “…asemapo uongo husema yaliyo yake mwenyewe kwa sababu yeye ni mwongo na baba wa huo…” haya yote ni mambo mabaya, ambayo chimbuko lake ni “mawazo hasi” yaliyomo katika “mfumo wa mawazo” katika akili za Ibilisi.

Sasa basi, ili kukujengea mtiririko mzuri wa uelewa katika hoja hii makini, sina budi kukujulisha pia kwamba, hata mambo ya kiroho yanayohusu  imani kwa Mungu, au kutokuamini Mungu nayo pia yako katika mfumo wa mawazo!

Biblia inaposema imani ni kuwa na hakika ya mambo yatarajiwayo, ni bayana ya mambo yalisiyoonekana, maana yake “hayo mambo yatarajiwayo” yako katika “mfumo wa mawazo”.

Mawazo huonekana akilini na rohoni tu. Na hakika juu ya mawazo yaliyoko moyoni nayo inategemea na akiba ya “mawazo ya Neno la Mungu” iliyoko ndani ya moyo wa mtu. Haya, hali ya “kutokuamini” nayo iko katika mfumo wa mawazo moyoni mwa mtu. Ndiyo! Kutokuamini ni akiba ya “mawazo hasi na yaliyo kinyume neno la Mungu”!

“Kutokuamini” ni “mtazamo kinyume na kufanikiwa kwa kutegemea njia za Mungu na kanuni zake”. Kwa hiyo, “Imani kwa Mungu” na “kutokuamini” vyote viko katika mfumo wa mawazo lakini, moja liko kwenye fungu la mawazo chanya kwamba ahadi za Mungu ni kweli na ndivyo ilivyo; na “kutokuamini” ni fungu la mawazo hasi yaliyojaa mashaka na wasiwasi juu ya uaminifu wa Mungu na ahadi zake.

Kupitia makala haya, tutakwenda kuchunguza ukweli kuhusu nguvu za mawazo, faida na athari zake katika maisha ya binadamu hapa duniani. Ngome za mawazo Sasa baada ya kupata utangulizi kuhusu tafsiri pana ya mawazo, mgawanyiko wake na chimbuko la mgawanyiko huo, ni bora sasa tuingie sehemu nzito kuhuzu mawazo ambayo yameitwa ngome katika maandiko matakatifu kama ilivyoanidkwa:  (maana silaha za vita vyetu si za mwili, bali zina uwezo katika Mungu hata kuangusha ngome;)

  tukiangusha mawazo na kila kitu kilichoinuka, kijiinuacho juu ya elimu ya Mungu; na tukiteka nyara kila fikira ipate kumtii Kristo; (2 KOR.10:4-5)

Hapa tumesoma maneno ya “silaha za vita”, “kuangusha ngome” na “kuangusha mawazo”. Kabla sijaingia uchambuzi wa ngome za mawazo hebu nitoe tafsiri ya msamiati wa neno “ngome”.  Ngome ni ukuta mnene uliojengwa kwa madhumuni ya kuzuia kuingia ndani, hasa maadui kuingia ndani kwa urahisi.

Kabla ya kuingia ndani ya mji/nyumba ili kupigana na kuteka waliomo/vilivyomo ndani kazi ya kwanza ni "kuangusha ngome za kuta” Haya, tuje kwenye tafsiri ya msamiati wa “ngome za mawazo” kwa mujibu wa maandiko tuliyosoma hapa juu. Kwa kifupi, maandiko yalichokuwa yana kilenga hapa ni

1.     “Falisafa za kibinadamu” zilizotungwa kwa kusudi la kupingana na elimu ya Neno la Mungu m.f nadharia ya mabadiliko inapopingana na “sayansi ya uuumbaji”

2.     “Nadharia potofu ya kidini” yaliyotungwa kupingana na kweli ya Neno la Kristo m.f hakuna kuokoka wala kuwa mtakatifu duniani, Roho na karama zake vilikwishakoma Kwa mujibu wa maandiko tuliyosoma, tunagundua mara moja kwamba Ibilisi ndiye mwasisi na mjenzi wa “ngome za mawazo” na mikakati yake siku zote ni kutanguliza mapema “Mawazo yake hasi” katika fahamu za watu ili kuwejengea “Falsafa za kibinadamu” zilizo kinyume na elimu ya Mungu pamoja na “mafundisho potofu ya kidini”

Hapa, kusudi la Ibilisi la kuwajengea mapema watu “ngome za mawazo” ni ili ziwazuie waathirika kuipokea Injili ya Kweli na Neno la Mungu (Biblia) na kupata kuokolewa na kujazwa Roho Mtakatifu. Na ndiyo maana sababu kubwa ya watu wengi kutokuiamini Injili sahihi ya wokovu ni kwa kuwa Shetani alitanguliza kwenye akili zao hizi i) Falisafa za uongo uliohalalishwa kijamii na ii) Injili za uongo zilizohalalishwa kidini!

Tutafanikiwa tu endapo tutazijua mbinu za Ibilisi
mara nyingi
huitumia NGOME YA MAWAZO
kama
silaha kuu.

MUNGU WANGU WA MBINGUNI AKUBARIKI KWA KUUSOMA UJUMBE HUU
naamini utakuwa umebarikiwa sana.
Ni mimi ndugu yako ktk Kristo
Ev. Elimeleck S Ndashikiwe

  elimelck@gmail.com
   0767445846 &
   0715445846

NGAO YA IMANI

UMUHIMU WA KUWEKA IMANI YAKO KATIKA JINA LA YESU KRISTO “Basi Petro na Yohana walikuwa wakikwea pamoja kwenda hekaluni, saa ya kusali , saa tisa. Na mtu mmoja aliyekuwa kiwete toka tumboni mwa mamaye alichukuliwa na watu, ambaye walimweka kila siku katika mlango wa hekalu uitwao Mzuri, ili aombe sadaka kwa watu waingiao ndani ya hekalu. Mtu huyu akiwaona Petro na Yohana wakiingia hekaluni aliomba apewe sadaka. Na Petro, akimkazia macho, pamoja na Yohana, akasema, Tutazame sisi. Akawaangalia, akitaraji kupata kitu kwao. Lakini Petro akasema, Mimi sina fedha, wala dhahabu, lakini nilicho nacho ndicho nikupacho. KWA JINA LA YESU KRISTO WA NAZARETI, simama uende. Akamshika mkono wa kuume, akamwinua, mara nyayo zake na vifundo vya miguu yake vikatiwa nguvu.

Akaondoka upesi akasimama, akaanza kwenda …” (Matendo ya Mitume 3:1 – 8) Ukifuatilia historia ya kilema huyu aliyeponywa utaona ya kuwa alikuwa hivyo tangu kuzaliwa, na alipopona alikuwa na umri uliopita miaka arobaini (M Na ndivyo ilivyokuwa wakati kilema huyu alipopona, watu waliokuwa hekaluni waliwashangaa wakina Petro na Yohana kama vile kilema huyo alipona kwa uwezo wao. Petro alipoona hali hiyo, aliamua kuwaeleza watu hao ukweli ulivyo; alisema hivi; “Basi (Yule aliyekuwa kilema) alipokuwa akiwashika Petro na Yohana, watu wote wakawakusanyikia mbio katika tao lile lililoitwa tao la Sulemani, wakishangaa sana. Hata Petro alipoyaona haya akawajibu wale watu, Enyi Waisraeli, mbona mnastaajabia haya, au mbona mnatukazia macho sisi, kama kwamba tumemfanya huyu aende kwa nguvu zetu sisi au kwa utauwa (utakatifu) wetu sisi?” (Matendo ya Mitume 3:11 – 12). Petro alikuwa anafanya jambo muhimu hapa kwa kusaidia kubadilisha mawazo ya watu ya kufikiria kuwa uwezo uliomponya kilema ulikuwa ni wa Petro na Yohana ambayo haikuwa si kweli. Kama uwezo huu haukuwa wao, muujiza huu siri yake ni nini? Petro aliendelea kusema hivi; “Mungu wa Ibrahimu na wa Isaka na wa Yakobo, Mungu wa Baba  zetu, amemtukuza mtumishi wake Yesu ….. Na kwa IMANI KATIKA JINA LAKE, JINA LAKE LIMEMTIA NGUVU  mtu huyu mnayemwona na kumjua; na imani ile iliyo kwake yeye imempatia huyu uzima huu mkamilifu mbele zenu ninyi nyote” (Matendo ya Mitume 3:13 – 16). Hebu tafakari maneno haya ya Petro; “Na kwa IMANI KATIKA JINA LAKE JINA LAKE LIMEMTIA NGUVU MTU HUYU….” Wakina Petro na Yohana waliweka imani yao katika jina la Yesu Kristo. Walikuwa na uhakika mioyoni mwao kuwa siri ya miujiza imo katika jina la Yesu Kristo – ndiyo maana  walipomkuta huyo kilema walimwamuru asimame kwa jina hilo! Weka imani yako katika jina la Yesu Kristo ukitaka kuona ishara na miujiza ya Yesu Kristo maishani mwako na kwa wale unaowahudumia pia. Wakijua hili wanafunzi wa kwanza wa Yesu Kristo walipokatazwa “wasiseme kabisa wala kufundisha kwa jina la Yesu” na Anasi kuhani mkuu, waliomba wakasema; “…Basi sasa, Bwana, yaangalie matisho yao; ukawajalie watumwa wako kunena neno lako kwa ujasiri wote, ukinyosha mkono wako kuponya; ISHARA NA MAAJABU vifanyike kwa JINA LA MTUMISHI WAKO MTAKATIFU YESU” (Matendo ya Mitume 4:18,29 – 31)      Ni muhimu kuwaeleza na kuwakumbusha watu umuhimu wa kuweka imani zao katika jina la Yesu Kristo wakitaka kuona mkono wa Bwana ukiponya, ukifanya ishara na miujiza. Nakumbuka kuna mama mmoja alifika nyumbani kwangu akiwa anaumwa sana toka mkoa mwingine nje ya mkoa huu wa Arusha ninaokaa. Baada ya mahojiano naye nilifahamu ya kuwa ameugua bila kupona kwa muda wa miaka miwili. Na katika miaka hiyo miwili amezunguka kwa watu mbalimbali kuombewa bila mafanikio. Alipoona haponi akaenda kwa waganga wa kienyeji ambako nako hakupona. Alipoona kwa waganga wa kienyeji haponi akaanza kutafuta watu wamuombee tena. Katika mazungumzo hayo nilitambua kuwa anapokwenda kuombewa anaweka imani yake katika watu wanaomuombea na wala haweki imani yake katika jina la Yesu Kristo. Nilifungua Biblia yangu na nikaanza kuzungumza naye juu ya uweza wa jina la Yesu Kristo, na umuhimu wa yeye kuweka imani yake katika jina la Yesu Kristo na siyo kwangu. Mwishoni nikamuuliza kama ameelewa na ikiwa yuko tayari kwa maombi kwa kulitumia jina la Yesu Kristo. Yule mama akajibu akasema; “Ndiyo nipo tayari kwa kuombewa, naamini kwa jina la Yesu Kristo nitapokea uponyaji” Mara nilipoanza kuomba, aliangushwa chini na mapepo yaliyojidhihirisha toka ndani mwake. Nikayaamuru mapepo hayo yamtoke mama yule kwa JINA LA YESU KRISTO – na mara hiyo yakamtoka na akawa mzima! Ugonjwa uliomsumbua kwa muda wa miaka miwili ulitoweka, yule mama pamoja na mume wake aliyemsindikiza waliondoka kwa furaha huku wakimsifu Mungu kwa matendo makuu aliyowatendea. Kumbuka Petro alisema; “… Kwa IMANI katika JINA LAKE (YESU) , JINA LAKE LIMEMTIA NGUVU MTU HUYU ….” Atakayeliitia jina la Bwana ataponywa : Nabii Yoeli alitabiri kuwa; “Na itakuwa ya kwamba mtu awaye yote ATAKAYELIITIA JINA LA BWANA ATAPONYWA; kwa kuwa …. Watakuwako watu watakaookoka, kama Bwana alivyosema;” (Yoeli 2:32).             Mtume Paulo alitilia mkazo utabiri huu aliposema;         “Kwa maana hakuna tofauti ya Myahudi na Myunani; maana yeye yule ni Bwana wa wote, mwenye utajiri kwa wote wamwitao; kwa kuwa, KILA ATAKAYELIITIA JINA LA BWANA ATAOKOKA (Warumi 10:12 – 13).             Kila anayeliitia jina la Bwana Yesu kwa imani anaponywa na, anaokoka kwa kuwa ndani ya jina hili la Yesu Kristo mna uponyaji na wokovu kwa kila amwaminiye Yesu Kristo. Lakini Mtume Paulo anauliza swali muhimu ambalo ni vizuri kulitafakari; anasema; “Basi wamwitaje yeye wasiyemwamini? Tena wamwaminije yeye wasiyemsikia? Tena wamsikieje pasipo mhubiri? (Warumi 10:14). Hili jambo ni kweli. Huwezi kumwita mtu usiyemwamini. Hii ina maana ya kuwa ikiwa tunataka watu waliitie jina la Yesu ili waokoke na kuponywa madhaifu yao, inatubidi tuhubiri na kufundisha juu ya Yesu na jina lake. Ndiyo maana Bwana Yesu Kristo alimwambia Anania ya kuwa Paulo “ni chombo kiteule kwangu, ALICHUKUE JINA LANGU, mbele ya Mataifa, na Wafalme, na wana wa Israeli” (Matendo ya Mitume 9:15). Biblia inasema pia kuwa; “Filipo akatelemka akaingia mji wa Samaria, AKAWAHUBIRI KRISTO. Na makutano kwa nia moja wakasikiliza maneno yale yaliyosewa na Filipo, walipoyasikia na kuziona ishara alizokuwa akizifanya kwa maana pepo wachafu wakawatoka wengi waliopagawa nao, wakilia kwa sauti kuu; na watu wengi waliopooza, na viwete, wakaponywa. Ikawa furaha kubwa  katika mji ule” (Matendo ya Mitume 8:5 – 8). Smithi Wigglesworth aliyekuwa mhubiri wa huko Uingereza katika miaka ya 1930 aliwahi kushuhudia katika mahubiri yake kuwa siku moja aliitwa kwenda kumuombea mgonjwa mmoja wa kifafa aliyekuwa amezidiwa hata kushindwa kuamka. Anasema watu wa eneo lile na hata ndugu zake yule mgonjwa walikuwa wamekata tamaa. Waliona ndugu yao atakufa kwa ugonjwa huo. Kwa hiyo ilimchukua muda Bwana Smith Wigglesworth kupata walio tayari kushirikiana naye katika kumuombea mgonjwa yule. Mwishoni alifanikiwa kuwapata, na anasema walikizunguka kitanda cha yule mgonjwa na wakaanza kuliitia jina la Yesu kwa pamoja wakisema “Yesu, Yesu, Yesu, Yesu,….” Kwa kulirudiaruda jina hili. Baada ya kuliitia jina la Yesu kwa muda hivi, anasema nguvu za Mungu zilishuka kitandani kwa yule mgonjwa, zikamtingisha mgonjwa na kitanda chake.             Yule mgonjwa akapona saa ile ile, akavaa nguo na kutoka nje. Kijiji kizima kilitaharuki na kushangaa kilipomuona mtu yule amepona. Smith Wigglesworth alipoona watu wamekusanyika hivyo wakishangaa, alichukua Biblia yake akahubiri, na watu wengi walikata shauri na kuokoka siku ile. Ni muhimu ufahamu ya kuwa muujiza unaofanywa kwa jina la Yesu Kristo unawavuta watu kwa Yesu Kristo, wamwamini na kumfuata.             Ndiyo maana imeandikwa juu ya Yesu Kristo kuwa;   “Hata (Yesu Kristo) alipokuwapo Yerusalemu kwenye sikukuu wakati wa Pasaka, watu wengi WALIIAMINI JINA LAKE, walipoziona ishara zake alizozifanya” (Yohana 2; 23). Siku moja nilikuwa katika sehemu fulani nikifundisha juu ya jina la Yesu Kristo. Mwisho wa somo nilisema watu wanaotaka kujazwa na Roho Mtakatifu na wanene kwa lugha mpya pamoja na wagonjwa waje mbele. Watu wengi walikuja mbele. Niliwaambia hatutaomba neno lolote zaidi ya kuliitia jina la Yesu kwa pamoja na kwa kulirudiarudia. Kwa pamoja tukaanza kuliitia jina la Yesu tukisema kwa sauti; “Yesu, Yesu, Yesu, Yesu…..” Muda haukupita mwingi, tukiwa bado tunaliitia jina hili nikasikia toka upande wangu wa kushoto sauti ya maji mengi yakiporomoka. Nilijua hii ni ishara ya uwepo wa Roho Mtakatifu kwani mahali tulipokuwapo hapakuwa na mto wowote karibu, wala mvua ilikuwa hainyeshi. Baadaye nilipowaeleza watu juu ya sauti hiyo ya maji, kuna wengine pia waliosema kuwa waliisikia. Tulipoendelea kuliitia jina la Yesu Kristo, wagonjwa walipona, waliokuwa na mapepo walipona, na wengine walijazwa Roho Mtakatifu na wakazungumza kwa lugha mpya. Ishara na miujiza mingi ilifanyika kwa kuliitia jina la Yesu Kristo. Kumbuka Yesu Kristo alisemal “Na ishara hizi zitafuatana na hao waaminio; kwa jina langu watatoa pepo, watasema kwa lugha mpya…” (Marko 16:17 –18). Hukumu kwa kutoliamini jina la Yesu : “Amwaminiye yeye hahukumiwi; asiyeamini amekwisha kuhukumiwa; kwa sababu HAKULIAMINI jina la Mwana pekee wa Mungu” (Yohana 3:18). Usipoliamini jina la Mwana pekee wa Mungu – jina la Yesu Kristo ujue umekwisha kuhukumiwa. Hii ina maana ya kuwa unapoteza wokovu; - unapoteza ushindi; - unapoteza uzima wa milele; - na pia bado unakaa katika mauti! Hebu soma na kutafakari mistari ifuatayo ili uone umuhimu wa kuliamini jina la Yesu Kristo: “Wapenzi, mioyo yetu isipotuhukumu, tuna ujasiri kwa Mungu; na lolote tuombalo, twalipokea kwake, kwa kuwa twazishika amri zake, na kuyatenda yapendezayo machoni pake. Na hii ndiyo amri yake, kwamba TULIAMINI JINA LA MWANA WAKE YESU KRISTO, na kupendana sisi kwa sisi, kama alivyotupa amri” (1Yohana 3:21 – 23). “Bali wote waliompokea (Yesu Kristo) aliwapa uwezo wa kufanyika watoto wa Mungu, ndio wale WALIAMINIO JINA LAKE” (Yohana 1:12). “Kwa maana kila kitu kilichozaliwa na Mungu huushinda ulimwengu; na huku ndiko kushinda kuushindako ulimwengu; hiyo imani yetu. Mwenye kuushinda ulimwengu ni nani, isipokuwa ni yeye aaminiye ya kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu? …. Na huu ndio ushuhuda, ya kwamba Mungu alitupa uzima wa milele; na uzima huu umo katika Mwanawe. Yeye aliye naye Mwana, anao huo uzima; asiye naye Mwana wa Mungu hana huo uzima. Nimewaandikia ninyi mambo hayo, ili mjue ya kuwa, mna uzima wa milele, ninyi MNAOLIAMINI JINA LA MWANA WA MUNGU”  (1Yohana 5:4-5; 11 – 13). “Wala hakuna wokovu katika mwingine awaye yote, kwa maana hapana JINA jingine chini ya mbingu walilopewa wanadamu litupasalo sisi kuokolewa kwalo” (Matendo ya Mitume 4:12) – isipokuwa ni JINA LA YESU KRISTO! MUHIMU : Kama tulivyokwisha kukuandikia katika sura ya tatu ya somo hili – ukitaka kulitumia jina la Yesu Kristo kihalali na uweze kuona uwezo na mamlaka yake ni muhimu: Kwanza:          Uwe mwana wa Mungu kwa kumpokea Yesu Kristo moyoni mwako kama Bwana na Mwokozi wako; Pili:                  Uwe mtii ukifuata maagizo ya neno la Kristo katika Roho Mtakatikfu. Kuna watu wengine wanataka kuwa watii kufuata maagizo ya neno la Kristo huku hawapendi kuokoka. Hawajui utii bila kuokoka ni utii nusu – ukitaka uone muujiza wa jina la Yesu Kristo katika maisha yako inabidi ufanye yote mawili – uokoke na utii. Ikiwa hujaokoka na unataka uokoke sasa isome sala ifuatayo kwa sauti (ikiwezekena upige magoti) mahali pa utulivu huku ukiamini ya kuwa Mungu anakusikia: “Ee Mungu wangu Mtakatifu. Nimesikia neno lako nami nimeamini. Naomba unisamehe dhambi zangu zote nilizokukosea katika maisha yangu yote. Damu ya Yesu Kristo iliyomwagika kwa ajili yangu, naomba initakase sasa katika roho yangu, nafsi yangu na mwili wangu. Nimefungua moyo wangu sasa; Ee Bwana Yesu Kristo nakuomba uingie ndani yangu, uwe Bwana na Mwokozi wangu kuanzia sasa na siku zote. Ahsante kwa kunisamehe dhambi zangu na Ahsante kwa kuniokoa. Amina” Ikiwa umeisema sala hii kwa imani, basi sasa wewe umeokoka na dhambi zako zimesamehewa na kusahauliwa na Mungu sawasawa na alivyoandika katika neno lake. Jina la Yesu Kristo ni halali yako kulitumia!